16 July 2014

WASIOJUA kuhusu uwezo wa asali na mdalasini wanaweza wasiamini wakiambiwa kuwa vina uwezo wa kuzuia na kutibu magonjwa hatari yaliyoshindakana hata hospitalini. Asali na mdalasini zimekuwa zikitumika kama tiba tangu enzi na enzi.

FAIDA ZA ASALI NA MDALASINI KIAFYA
Asali na mdalasini bado inaendelea kutumika kama tiba katika magonjwa ya aina mbalimbali, hasa kwa baadhi ya watu wanaoamini katika tiba mbadala kuliko tiba za kisasa, na kwa kiwango kikubwa wameweza kutibu maradhi yao bila kupata athari zingine.

Kwa mujibu wa tafiti mbalimbali za kisayansi, asali ina dawa asilia ya kuua vijidudu mwilini (anti- bacterial properties). Kama ukiweka asali kwenye kidonda au mahali ulipoungua na moto, utazuia maambukizi na utaponya kidonda pia.

Ulaji wa mara kwa mara wa asali na mdalasini kwa pamoja, hutoa kinga dhidi ya ugonjwa wa moyo, kwani vyakula hivi husafisha mishipa ya damu na huyeyusha mgando wa damu kwenye mishipa. Kuziba kwa mishipa huwa ndiyo chanzo cha tatizo la shinikizo la damu na magonjwa ya moyo.

Unywaji wa asali iliyochanganywa na mdalasini kwenye maji ya uvuguvugu, utasaidia kusafisha kibofu cha mkojo na hivyo kuondoa maambukizi yoyote yanayoweza kuwepo kwenye kibofu. Kwa maana nyingine, kwa kupenda kunywa mchanganyiko huo, utajiepusha na matatizo ya kuziba kwa haja ndogo na hata saratani ya kibofu kwa kukiweka kibofu chako salama kila wakati.

Aidha, unywaji wa mara kwa mara wa mchanganyiko huo, hutoa nafuu kubwa ama huweza kuponya kabisa wenye matatizo ya ugonjwa wa baridi yabisi (arthritis). Mgonjwa anywapo mchanganyiko huu, maumivu hutoweka mara moja na kumpa nafuu ya haraka.

Vilevile, unywaji wa mchanganyiko wa asali na mdalasini huimarisha kinga ya mwili na huweza kuondoa magonjwa yote ya kuambukiza kama vile mafua au flu na huondoa mwilini baadhi ya vijidudu vinavyoambukiza magonjwa mbalimbali. Ukitengeneza mchanganyiko mzito wa asali na mdalasini na kupakaa kwenye jino linalouma utapata nafuu haraka na utazuia pia kuendelea kuuma kwa jino.

Asali na mdalasini ikitumiwa kwa pamoja pia, husadia usagaji wa chakula tumboni na hivyo kuwezesha upatikanaji wa choo laini na huzuia tumbo kujaa gesi. Asali na mdalasini pia huongeza nguvu mwilini na huchangamsha ubongo na kumfanya mtu kuwa mchangamfu kazini.

Kuna tafiti nyingine zinaonesha kuwa asali na mdalasini humuwezesha mtu kupunguza uzito kirahisi na ni kinga imara dhidi ya baadhi ya saratani. Hata hivyo, inashauriwa kutegemea vyakula hivi maarufu katika kutoa kinga ya maradhi kuliko kutegemea kama tiba zaidi, kwani kwa baadhi ya magonjwa sugu haviwezi kuponya kwa haraka.

Ili kupata faida ya asali na mdalasini kama kinga, ni vizuri kuzingatia kanuni za ulaji sahihi kwa ujumla na kutumia vyakula hivi kama sehemu ya mlo wako wa kila siku sambamba na vyakula vingine sahihi, huku ukizingatia suala la kuushughulisha mwili kwa mazoezi na kazi.

0 comments:

Post a Comment

.

Subscribe to RSS Feed Follow me on Twitter!